
Ujiimarishaji wa eneo la hifadhi ya jadi Kawawana
Mageuzi ya mwongozo huu yalianza zaidi ya muongo mmoja uliopita: Wamiliki/wanufaika wa eneo la hifadhi ya jadi la Kawawana nchini Senegali walikuwa wakikabiliwa na matishio makubwa kwa pamoja katika eneo lao la jadi na vipato vyao vya kujikimu. Walielewa kuwa ili kushughulikia matishio hayo, ‘eneo lao la hifadhi ya jadi’ lilikuwa kipaumbele na lilihitaji kurejeshwa kwenye hali yake ya asili. Kwa sababu hiyo, pia kwa mila na kanuni zao za jadi juu ya kupata na kuzitumia maliasili, zilizounganishwa na uelewa mpya na zana, zilihitajika kutambuliwa zaidi na kuheshimiwa. Hiki ndicho walichofanikisha! Walifanyaje? Walishiriki katika mchakato wa kutafakari, kujadiliana, na kuchukua hatua: ‘mchakato wa kujiimarisha wenyewe’.
Wamiliki/wanufaikaji wa eneo la hifadhi ya jadi Kawawana walianza mchakato wao wa kujiimarisha wenyewe mwishoni mwa mwaka 2008. Hadithi yao inaonyesha nguvu ya mchakato kama huo na kutoa mfano wa jinsi ya kufanya.
Mchakato wa kujiimarisha wenyewe ulianza mwishoni mwa mwaka 2008, wakati neno Kawawana halikuwepo na eneo la mto lilikuwa katika hali mbaya sana. Katika mkutano wa awali kati ya viongozi wa manispaa ya Mangagoulack vijijini, wawakilishi wa shirika la wavuvi wenyeji, na wageni kutoka Muungano wa Kongani la Kitaifa, walijadili hali zote zilizokuwa na ugumu. Walikubaliana kwamba eneo lao lilihitaji kurejeshwa ili kuleta staha na kipato cha kujikimu kwa jamii. Kwa maoni yao, hili lingeweza kufanyika tu ikiwa jamii ingeweza kuzirejesha kanuni zake za jadi za kuzifikia na kuzitumia maliasili. Kanuni za jadi zingekomesha uporaji wa wazi wa maliasili uliokuwa ukifanyika mbele ya macho yao na mtu yeyote anayeweza kuvua, kukata miti, au kukusanya chochote ndani ya eneo lao. Kwa hali hiyo, uungwaji mkono wa serikali ulikuwa muhimu sana… Wote walijua kwamba kiongozi wa jamii ya jirani yao alifungwa jela kwa kujaribu kutekeleza sheria ya kanuni za uvuvi za mila bila ya kushirikisha serikali. Hivyo waliogopeshwa na hilo, na hawakuona njia ya kuwatoa kwenye hiyo hofu bila ya kushirikisha serikali.
Kwa mamlaka thabiti kutoka kwa washiriki wote katika mkutano wa awali, wageni kutoka Muungano wa Kongani la Kimataifa waliweza kwa haraka kupata rasilimali za kusaidia mchakato wa kujiimarisha kwa jamii. Mapema mwaka 2009, walianza na mikutano kwa majuma matatu mfululizo na kila juma walifanya mikutano miwili wakijadili kwa kina kati ya wawakilishi 150 kutoka vijiji nane vinavyojuisha jamii hiyo. Mikutano ilikuwa kama isiyo rasmi lakini yenye malengo/maono na umakini mkubwa kuanzia mashinani, na watu kutathmini hali halisi, kuweka maono/dira ya kile wanachotamani kukipata na kupanga nini cha kufanya. Mchakato huo ulifanikishwa na timu ya washauri watatu wa nje ya jamii, ikijumuisha mtaalamu wa uvuvi, uchumi wa kilimo na pia mtaalamu mshauri wa utawala na uwezeshaji wa mchakato mzima.
Hapo awali, kikundi cha wavuvi zaidi ya ishirini wenye uzoefu na kuheshimiwa kutoka vijiji vinane walikusanyika ili kuchambua hali ya sasa na kihistoria ya uvuvi hapo kijijini, na kuyaelezea matukio na mwelekeo wa utofauti ya ukubwa na idadi ya samaki waliovuliwa. Kisha kundi lingine kubwa la wawakilishi wa kijiji lilijiunga kusikia kutoka kwa wavuvi hao. Kwa pamoja, walikumbushana historia ya jamii yao, uhusiano wao wa kina kitamaduni na kimila katika eneo lao (utamaduni wa Djola ni mpana na una utajiri kama mtu anavyoweza kufikiria) na hali yao ya sasa ya kiikolojia na kijamii na kiuchumi. Wakiambatana na kundi kubwa kutambua mustakabali wanaoutamani au walichomaanisha waliposema wanataka “maisha mazuri” (Bourong Badiaké). Ilibainika kuwa walichomaanisha wote ni amani, mshikamano wa jamii, ustawi, lishe bora zaidi, kuzuia idadi kubwa watu kwenda mijini, na mazingira mazuri na yenye tija. Kwa haya yote, walitambua kwamba eneo lao la jadi- ambalo waliliita Kawawana au “urithi wetu wa pamoja wa asili wa kuhifadhiwa na sisi sote”– lilikuwa muhimu. Kupitia majadiliano na uchambuzi zaidi, wote walikubali kwamba walihitaji kurejesha Kawawana yao kupitia kutambuliwa na kuheshimiwa kwa kanuni zao za kitamaduni (zilizounganishwa na zana za kisasa za ufuatiliaji wa kibaolojia). Hatimaye, waliamini kwamba hii ndiyo sababu moja muhimu zaidi itakayoleta matokeo yote mazuri ya maisha ambayo waliyatamani. Ufahamu huu ulikuwa wakati muhimu sana kwa wote waliohusika.
Kwa haya yote, walitambua kwamba eneo lao la jadi – ambalo waliliita Kawawana au “urithi wetu wa asili wa kuhifadhi wenyewe”– ulikuwa muhimu.

.
Wakati majadiliano haya yakifanyika, kikundi cha wavuvi cha awali kilikuwa kikipata mafunzo ya ufuatiliaji wa kibaolojia na kikundi kingine kinachoitwa Kaninguloor kiliundwa ili kujadili viashiria vya kuonyesha mabadiliko yanayotarajiwa kuelekea “maisha bora” (Bourong Badiaké) na jinsi viashiria hivyo vinaweza kutathminiwa. Timu hizo mbili zilizojitolea (kikundi cha ufuatiliaji wa uvuvi na kikundi cha Kaninguloor) walikubaliana kuendelea kupima na kutathmini aina mbili za viashiria vilivyochaguliwa, kufuatilia kama vingekaribia mabadiliko yaliyotarajiwa, ikiwa ni lini na wakati gani kanuni zao za jadi zingepaswa kurejeshwa.

.
Kisha kwa pamoja walipanga kile walichohitaji kufanya. Kimsingi, walihitaji maarifa na kanuni zao za kiasili za kutambuliwa rasmi na kuheshimiwa katika upatikanaji na matumizi ya maliasili yao. Kwa hiyo, waliamua kuianzisha Kawawana kuwa ‘eneo lao la hifadhi yao ya jamii’ na kujitahidi kuhakikisha linatambuliwa rasmi. Taarifa zilizopokelewa kutoka kwa Muungano wa Kongani la Kimataifa ziliifahamisha jamii kuhusu baadhi ya kanuni za kitaifa na kimataifa na misingi ya sera ambazo zitafanya eneo lao lililohifadhiwa liweze kutambuliwa. Hizi ni pamoja na Sheria ya Senegal ya Ugatuaji, pamoja na hadhi ya nchi kuridhia maamyzi ya Mikataba ya Bioanuwai, ambayo inapendekeza kusaidia uhifadhi wa maliasili za kijamii. Habari hii ilikuwa muhimu, na iliiwezesha jamii kujiamini ili kuchukua hatua. Wawakilishi 150 walitumia muda wao kutengeneza na kukubaliana juu ya mpango wa usimamizi wa eneo lililohifadhiwa la jamii (pamoja na kanda tofauti, kanuni, alama, ufuatiliaji, na adhabu kwa ukiukwaji wowote ule); muundo wa utawala (wenye majukumu mbalimbali kwa taasisi mbalimbali); mfumo wa ufuatiliaji kwa utawala na matokeo ya usimamizi; mpango wa mawasiliano; na mipango ya nyongeza kuboresha kipato cha kujikimu, kusaidia shughuli za wanawake, kuwatambua waungaji mkono na washirika katika ngazi mbalimbali na kutafuta kutambuliwa rasmi kwa eneo hilo lililohifadhiwa la jamii.
Katika miezi kumi na minane iliyofuata, yote yaliyokuwa yamepangwa yalitekelezwa. Sababu muhimu ilikuwa baadhi ya viongozi wachache kufanya kazi bila kuchoka kama wanadiplomasia wa jamii, kwa akili na uamuzi na uungwaji mkono na jamii. Baada ya kutambuliwa rasmi na manispaa ya Mangagoulack vijijini mwaka 2009, kazi ya kubadilishana taarifa na uchechemuzi iliendelea kwa miezi mingi katika idara za uvuvi na misitu na nyingine nyingi. Hatimaye, hata hivyo, mwezi wa tatu na sita mwaka 2010, Kawawana ilipata vyeti vya kutambuliwa rasmi kutoka Halmashauri ya Mkoa na Gavana wa Casamance. Huu ulikuwa utambuzi kamili na rasmi ambao waliweza kufikiria kuupata! Jamii ilisherehekea matokeo haya kwa dhati, kwa kuanzia na wanawake wenye umri mkubwa na busara zaidi kuonesha vitu kuashiria maeneo tofauti, na kanuni za uvuvi. Kisha wanaume waliweka nguzo ya msingi na jukwaa kwenye maeneo yaleyale kama alama zenye maelezo maalumu kuhusu kanuni za uvuvi. Na hatimaye, kila mtu katika jamii ambaye aliweza kuhudhuria tukio/sherehe hiyo kubwa alifanya hivyo, ambapo mamlaka na washirika walikuja kutangaza kuanza kutumika rasmi kwa kanuni za Kawawana. Hii ilihusisha hotuba, chakula, muziki na furaha kwa ujumla.
Hatimaye, hata hivyo, mwezi wa tatu na wa sita mwaka 2010, Kawawana ilipata vyeti vya kutambuliwa rasmi kutoka Halmashauri ya Mkoa na Gavana wa Casamance. Huu ulikuwa utambuzi kamili na rasmi zaidi ambao wangeweza kufikiria kuupata!
Wakati jamii ikitafuta utambuzi rasmi, vivyo hivyo ilikuwa ikitafuta msaada wa kutekeleza mpango wao wa usimamizi. Wakati kanuni za usimamizi zinaridhiwa rasmi, ziliendelea kutekelezwa kwa urahisi kwa msaada wa mashua ndogo yenye injini na vifaa vya ziada vilivyotolewa kwa msaada wa Wakfu wa FIBA. Kikosi cha doria ya kufuatilia kanuni zilizowekwa haikuwa rahisi kila wakati, na baadhi ya migogoro ilisababishwa na wavuvi wasio wenyeji, lakini Wakala wa Uvuvi na Kiranja wa ufuatiliaji waliiunga mkono timu ya doria na wanadiplomasia walifanya yaliyosalia. Kwa kuimarisha jukumu lao, wavuvi wa kujitolea kwenye timu ya doria walikusanya rasilimali ili kujilipia baadhi ya mafunzo kutoka kwa wakala wa serikali wa uvuvi, ili baada ya hapo wakachukuliwe kama mawakala wasio rasmi. Wakati Wakfu wa FIBA ukitekeleza malengo ya uhifadhi, iliomba jamii pia kuunda timu ya ufuatiliaji wa bioanuwai isiyo ya samaki, ambapo iliundwa mara moja.

.
Chini ya miaka mitatu baada ya kutambuliwa rasmi kwa eneo lililohifadhiwa la jamii, timu zote za ufuatiliaji zilionyesha matokeo mazuri sana. Uvuvi na bioanuwai ya eneo hilo ilionyesha mabadiliko ya kuridhisha (aina tofauti tofauti za samaki wa awali zilijitokeza tena, ndege, pomboo na mamba waliongezeka kwa wingi na baadhi ya wavuvi walisema upatikanaji wa samaki uliongezeka mara nne!). Viashiria vya ustawi wa jumla pia vilibadilika, kuhusu uhamiaji (watu wachache walihama na wengine walirudi vijijini) na lishe (watu walikuwa wanakula vizuri tena samaki waliowapenda, ambao walikaribia kutoweka katika eneo lao). Viashiria vingine vya Bourong Badiaké kwa ulinganifu, vilikuwa pia vizuri kiasi, lakini havikuwa pia vibaya hapo mwanzoni na vilionekana kutokuwa na ‘unyeti’ kuliko aina nyingine yoyote ya mabadiliko.
Katika miaka iliyofuata, baraza kuu la uongozi la Kawawana liliendelea kukutana kushughulikia masuala mbalimbali, na iliendelea kufanya kazi yenyewe, bila msaada wa mradi. Kulikuwa na jaribio la kutafuta fedha kwa ajili ya Kawawana kupitia biashara ndogo ya kukodisha baiskeli, lakini biashara ilionekana kuwa ngumu sana na ikiwa inatumia muda mwingi kwa wananchi wanaojitolea kwa hiari. Hata hivyo eneo lililohifadhiwa la jamii lilipanuliwa kwa hiari. Lakini ni wazi kuwa kutawala na kusimamia eneo lililohifadhiwa la jamii kwa hiari tu na kujitoa mno kwa watu ambao hawana muda au rasilimali za ziada lilihitaji moyo. Kwa mfano, kikosi cha doria cha Kawawana kwa sasa kinakabiliwa na tatizo kwa sababu injini ya mashua yao ya doria ambayo ni sehemu ya vifaa muhimu vya ufuatiliaji imeharibika katika ajali iliyosababishwa na hali mbaya ya hewa. Watu wa eneo hilo wanatafuta rasilimali ili kutafuta kipato cha kujikimu. Hakuna mtu anayeweza kusema ni kwa muda gani juhudi zao za kujitolea zitaendelea.
Kiasi kidogo cha fedha kilichopokelewa mara kwa mara kutoka Kongani la Kitaifa kililenga mipango ya ubunifu, kama vile kipindi cha redio katika lugha ya asili, ambacho kimewafanya Kawawana kujulikana sana na kuheshimiwa. Kutambuliwa huku siyo kwa wenyeji tu. Kawawana imepokea tuzo mbili za kimataifa kwa mafanikio yake na kuhamasisha jamii nyingine kuwa wamiliki wa maeneo yao yaliyohifadhiwa nchini Senegal.
Kwa pamoja, na kwa msaada wa ruzuku nyingine ya Mpango wa kimataifa wa kusaidia Muungano wa Kongani la Kimataifa, wamiliki wa jamii wa maeneo ya hifadhi ya jadi nchini Senegal wametengeneza mtandao wa kitaifa. Wakati wa andiko hilo, mnamo 2020, mtandao wa kitaifa ulianza ushawishi wa kuwa na sera za kitaifa za kuunga mkono rasmi maeneo ya jamii yaliyohifadhiwa na kuimarisha usalama wao. Hata hivyo, kazi ya ushawishi bado haina nguvu, na ushauri wa kisheria unahitajika.
Katika kipindi chote cha mchakato wa miaka kumi na miwili iliyoelezwa kwa ufupi hapo juu, jamii ya wamiliki ya Kawawana imekuwa ukiuimarisha mchakato wa usimamizi kuimarisha eneo lake la jadi. Mwanzo ulikuwa mgumu wa kuimarisha, ila mwendelezo umekuwa wa kuridhisha. Jamii yenyewe ilianza kujiimarisha kwa kujikumbusha hali yake halisi ilivyokuwa, kuichambua hali ilivyo ilivyo kwa wakati huo, kuiwekea kumbukumbu zote, kujijulisha, kukubaliana hatua za kuchukua, kupanga na kujitoa kwa pamoja, kuunganisha mahusiano na waungaji mkono na washirika, kufanya kazi ya kidiplomasia kwa uangalifu, kukubalika, kutambuliwa na kuungwa mkono na kusherehekea mafanikio yake. Kisha iliendelea kuimarika kwa kufanya kazi pamoja kwa miaka mingi, kutawala na kusimamia eneo lao, na kufunzwa ujuzi mpya, kuwasiliana kuhusu eneo lao la jadi, kujifunza, kushirikiana mafunzo na jamii nyingine na kutafuta njia za kuboresha muktadha wa jumla wa sera nchini Senegal. Uwezeshwaji kutoka nje na msaada katika nyakati muhimu imekuwa muhimu, lakini sehemu kubwa ya michango na juhudi zimepatikana ndani ya nchi. Leo, jamii ya wamiliki ya Kawawana haijatatua matatizo yake yote kwani ina misukosuko yake kama jamii nyinginezo… lakini ina nguvu zaidi kuliko miaka kumi iliyopita, na eneo lake la jadi ni lenye afya na hai!
Photos © Grazia Borrini-Feyerabend